Mkuu wa Wilaya ya Urambo Mhe. Dkt. Khamis Athuman Mkanachi amefungua Kituo Jumuishi cha kutoa huduma kwa waathirika wa ukatili wa kijinsia(One Stop Center) katika Wilaya ya Urambo, ili kuhakikisha wahanga wa matukio ya ukatili wa kijinsia wanapata mahala pa kupata msaada na Faragha zao kulindwa.
Uzinduzi huo umefanyika katika Hospitali ya Wilaya ya Urambo tarehe 24.06.2025, katika jengo la wagonjwa wa nje (OPD) ambapo ndipo Huduma Jumuishi (One Stop Center) ilipo.
Uzinduzi huo umehudhuriwa na Wadau mbalimbali wakiwemo Kamati ya Ulinzi na Usalama Wilaya, Mkurugenzi mtendaji aliyeambatana na baadhi ya Watumishi wa Halmashauri, Viongozi wa Vyama vya Siasa, Viongozi wa Dini na Wadau na Taasisi za umma na Binafsi.
Katika uzinduzi huo Mhe. Dkt. Mkanachi amesema kuwa, wadau wote wanapaswa kuwa mabalozi kwa wananchi ili kufikisha ujumbe juu ya uwepo wa Kituo jumuishi katika Hospitali ya Wilaya kwa ajili ya kuwahudumia wahanga wa matukio ya ukatili ili wananchi wa Urambo waweze kutumia kituo hicho.
Aidha Mhe. Dkt. Mkanachi amesema kuwa, kwa sasa mmonyoko wa maadili umekithiri sana kwani hatari ya matukio ya ukatili wa kijinsia ni kubwa kwa makundi mbalimbali walengwa wa matukio hayo.
Ameeleza kuwa maeneo yaliyokuwa yanatarajiwa kuwa salama nayo yameripotiwa kuwa na matukio hayo, hivyo ni wajibu wa kila mtu kuweka nguvu ya pamoja kuandaa mazingira salama ya kupunguza matukio hayo pamoja na kutumia kituo hicho pale ambapo matukio yanajitokeza.
Mhe. Dkt. Mkanachi aliueleza Umma uliojitokeza kushuhudia ufunguzi huo kuwa, sababu kubwa yakuanzisha kituo hicho ni kuondoa Usumbufu na hofu kwa Wananchi wanaokutana na Ukatili katika uwasilishwaji wa Matatizo yao kwani awali huduma ilikuwa haipatikani sehemu moja, hivyo ilimlazimu mhanga kupita maeneo mbalimbali.
Aidha Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Urambo Bi. Grace Quintine amesema kuwa, Katika Jamii kuna matukio mengi ya ukatili wa kijinsia hivyo amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyekuja na wazo la kuanzishwa kwa vituo jumuishi katika vituo vya kutolea huduma za Afya, hali inayosaidia katika uboreshawaji wa utoaji wa huduma kwa wananchi.
Akizungumza katika ufunguzi huo Mganga Mkuu wa Wilaya ya Urambo Dkt. David Manyama amesema kuwa, Kituo hicho kinajumuisha maafisa Ustawi wa Jamii, Polisi, Daktari na wataalamu wengine muhimu ambao watamsaidia mhanga kuweza kupata huduma stahiki.
Bomani Urambo
Anunani ya posta: Mkurugenzi Mtendaji (W), 30 Br ya Boma Stendi, S.L.P 170. 45582 Urambo Tabora
Simu ya mezani: +255 (0) 262 965 824
Simu ya mkononi: DED GRACE:0786821141
Barua pepe: ded@urambodc.go.tz
Copyright ©2025 Urambo . All rights reserved.